
Mamlaka ya Mawasiliano nchini Uganda, UCC, imeamuru
kufungwa kwa mitandao ya kijamii ikiwa zimesalia siku mbili tu kufanyika kwa
uchaguzi mkuu nchini humo, gazeti la Daily Monitor limeripoti.
Katika barua yake, Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Bi
Irene Sewankambo ameagiza kampuni za mawasiliano nchini humo "kufunga kwa
haraka upatikanaji na matumizi" ya mitandao ya kijamii. Watumiaji nchini
humo wameripoti kushindwa kutumia mtandao wa Facebook, Twitter WhatsApp na
Signal tangu asubuhi, huku upatikanaji wa AppStore, PlayStore na YouTube ukiwa
na changamoto pia.
Chanzo cha habari kinaeleza kuwa mamlaka ya mawasiliano
imetoa zaidi ya VPN 100 kwa makampuni ya mawasiliano kwa ajili ya kuhakikisha
kuwa zinafungiwa nchini humo.
Mamlaka hiyo, hata hivyo, imekana kutoa agizo la kufunga
mawasiliano kupitia msemaji wa UCC, Ibrahim Bbosa.
"Kumekuwa na tatizo la muunganiko hafifu wa intaneti,
lakini inaweza kuwa ni kutokana na kuongezeka kwa watumiaji wakati tunaelekea
katika zoezi la uchaguzi," Bbosa aliwaambia wanahabari.
Hatua hii inakuja kufuatia kauli ya Waziri wa Ulinzi na
Masuala ya Maveterani kuwaambia wanahabari kuwa serikali inatafuta namna bora
ya kudhibiti mitandao ya kijamii, ikidai kuwa inatumika vibaya wakati huu wa
uchaguzi.
Mtandao wa Facebook umethibitisha siku ya Jumatatu kuwa
umefungia baadhi ya akaunti za serikali ya Uganda kutokana na kutumiwa vibaya
kwa akaunti hizo kushawishi maamuzi ya umma.
Mkuu wa Mawasiliano wa Facebook wa Ukanda wa Nchi za
Kusini mwa Sahara, Kezia Anim-Addo amesema kuwa Facebook imechukua hatua hiyo
baada ya kujiridhisha kuwa baadhi ya akaunti za mtandao wa Facebook
zimejihusisha katika jaribio la makusudi la kushawishi maamuzi ya umma,
wakilenga mdahalo unaotarajiwa kufanyika kabla ya uchaguzi.
"Wametumia akaunti feki kuendesha kurasa na kuandika
maoni katika machapisho ya watu, wakijivika uhusika wa watu wengine na
kusambaza machapisho katika makundi na kuyafanya kuwa maarufu kuliko
yalivyotakiwa kuwa," Kezia Anim-Addo alisema katika barua pepe, akiongeza
kuwa mtandao wa akaunti hizo unahusishwa na Wizara ya Habari na Mawasiliano ya
Uganda.
Hii ni mara ya pili kwa serikali ya Uganda kufungia
mitandao ya kijamii, ambapo mwaka 2016, serikali ilifungia mtandao wa Facebook
na Twitter kabla ya mgombea wa urais na mshindani wa Rais Museveni kuwahimiza
wananchi kutumia VPN.
Leave a comment