
Jerry John Rawlings aliyekuwa Afisa wa Jeshi na mwanasiasa nchini Ghana, aliongoza mapinduzi mawili ya kijeshi kabla ya kuongoza nchi yake kuelekea utawala wa Kidemokrasia. Ameaga dunia Jumanne ya Novemba 12, 2020 akiwa na miaka umri wa 73.
Jerry alizaliwa mwaka 1947, na mauti yake
yamemkuta akiwa katika hospitali ya Korle Bu huko katika jiji la Accra
nchini Ghana akipatiwa matibabu baada ya kuugua kwa muda mfupi.
Rais Nana Akufo-Addo amesema “mti mkubwa umeanguka, Taifa la Ghana limepoteza kitu cha thamani sana”. Rais Nana ametoa pole kwa familia ya marehemu na kutangaza bendera zote kupepea nusu mlingoti kwa siku saba huku nchi hiyo ikijiandaa na shughuli za msiba huo.
Hayati Rawlings alizaliwa na baba Mskochi huku mama
yake akiwa Mghana ambaye naye alifariki mwaka huu akiwa na umri wa miaka 101.
Rawlings alikuwa ni mwanajeshi aliyebobea kwenye masuala ya anga akiwa ni
rubani mahiri katika kurusha ndege za kivita ambapo mwaka 1969 alitukunukiwa
tuzo ya “Speed Bird Trophy” baada ya kufanikiwa kurusha ndege ya kivita aina ya
Su-7.
Mwaka 1978 alikabidhiwa cheo cha Uluteni katika
Jeshi la Anga la Ghana, ilipofika mwaka 1979 Hayati Rawlings akiwa na wanajeshi
wengine sita waliongoza mapinduzi ya kijeshi dhidi ya utawala wa kijeshi wa
Jenerali Fred Akuffo ambaye aliingia madarakani mwaka 1978, mapinduzi hayo
hayakufanikiwa hali iliyopelekea yeye pamoja na wenzake kukamatwa na
kufunguliwa mashtaka kwenye mahakama ya kijeshi ambako alihukumiwa adhabu ya
kifo. Lakini kauli zake za kishujaa kuhusu hali ngumu ya maisha kabla ya
kukamatwa zilimpatia wafuasi wengi.
Juni 4, 1979 akiwa anasubiri siku ya hukumu yake ya
kifo kufika alikombolewa gerezani na kundi la wanajeshi waliovamia gereza
alikofungwa. Akiwa ameshikilia ajenda ya rushwa iliyokithiri kwenye serikali ya
Jenerali Fred Akuffo na kwamba serikali mpya inahitajika ili kuleta mageuzi na
maendeleo ya kweli, aliongoza kikundi cha wanajeshi ambao walimpindua Jenerali
Akuffo na uongozi wake.
Baada ya mapinduzi hayo aliunda kundi lenye wajumbe
15 lililoitwa Armed Forces Revolutionary Council (AFRC), na
walitawala kwa siku 112 wakapanga mauaji ya halaiki ya wanajeshi 8 wenye vyeo
vya juu watatu kati yao walishakuwa wakuu wa nchi hiyo, Afrifa, Acheampong, na Akuffo.
Septemba 24, 1979 alikabidhi madaraka kwa utawala
wa kiraia wa Rais Hilla Limann kutoka chama cha PNP ambacho kilikuwa kinaungwa
mkono na wafuasi wa Rais wa kwanza wa Taifa hilo Kwame Nkurumah. Miaka miwili
baadaye, Desemba 31, 1981 Rawlings aliongoza mapinduzi ya kijeshi dhidi ya Rais
Hilla Limann akidai utawala wa Rais huyo ulikuwa dhaifu na uchumi wa nchi hiyo
ulikuwa kwenye hali mbaya.
Rawlings alianzisha chama chake kilichoitwa PNDC
ambacho kilileta sera mbalimbali za mageuzi ya kiuchumi ambayo hazikuwa na
mafanikio sana. Kufikia mwaka 1983 Taifa hilo lilikumbwa na mgogoro wa kiuchumi
ambao mabadiliko ya kimfumo hali iliyomlazimu kuitisha uchaguzi wa kwanza
wa vyama vingi na ukafanyika mwaka 1992.
Katika utawala wake alianzisha mchakato wa Katiba
mpya na kufanikiwa kuandika Katiba mpya ya Kidemokrasia iliyoruhusu vyama vingi
na uundwaji wa Tume huru ya uchaguzi. Katiba hiyo iliweka ukomo wa Urais kwa
kuweka vipindi viwili vya Urais vya miaka mitano.
Kwa mujibu wa Katiba hiyo mpya ya utawala wa kiraia
kipindi chake cha uongozi kilifikia mwisho mwaka 2001 ambapo alistaafu na
nafasi yake kuchukuliwa na John Agyekum Kufuor mpinzani wake mkuu kwenye
uchaguzi wa 1996.
Baada ya kustaafu aliteuliwa kwenye kazi kadhaa za
Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika ikiwemo Mjumbe maalumu wa AU kwa nchi ya
Somalia.
Jerry Rawlings atakumbukwa kama Rais aliyeweka
misingi ya kidemokrasia katika Taifa la Ghana kwa kuruhusu mfumo wa vyama vingi
na mchango wake katika kuleta Katiba mpya ya kwanza ya vyama vingi ambapo kwa
sasa Ghana inatajwa kama moja ya nchi kwenye Ukanda wa Afrika ya Magharibi
ambayo Demokarasia yake imekomaa.
Akiwa Rais pia atakumbukwa kwa kuhimiza uwekezaji
kwenye sekta za mafuta na dhahabu. Pia atakumbukwa kwa kuikuza taswira ya Ghana
Kimataifa kwa kupeleka wanajeshi wake kwenye vikosi vya Umoja wa Mataifa kwenye
kulinda Amani kwenye nchi za Liberia, Sierra Leone, Lebanon na Iraq.
Hayati Jerry John Rawlings ameacha mjane, Nana Konadu Agyeman, watoto wa kike watatu, Zanetor Rawlings, Yaa Asantewaa Rawlings, Amina Rawlings; na wakiume mmoja, Kimathi Rawlings.
Leave a comment